Juma kuu
From Wikipedia, the free encyclopedia
Juma kuu (kwa Kilatini: Hebdomas Maior, lakini kwa kawaida zaidi Hebdomas Sancta yaani "Wiki Takatifu"; kwa Kigiriki: Ἁγία καὶ Μεγάλη Ἑβδομάς, Hagia kai Megale Hebdomas, "Juma Takatifu na Kuu") ni juma la mwaka ambalo Wakristo wanaadhimisha kwa namna ya pekee matukio makuu ya historia ya wokovu kadiri ya imani yao, kuhusiana na mwisho wa maisha ya Yesu huko Yerusalemu, uliofuatwa na ufufuko wake.
Katika madhehebu mengi ya Ukristo, juma hilo linaanza na Jumapili ya matawi ambapo linaadhimishwa kwa shangwe tukio la Yesu Kristo kuingia huo mji mtakatifu kama mfalme wa Wayahudi huku akipanda punda na kushangiliwa na umati wa wafuasi wake, waliofurahia hasa alivyomfufua Lazaro wa Betania.
Lakini Yesu alieleza kuwa ufalme wake si wa dunia hii, na kuwa yeye hakuja kutumikiwa bali kutumikia na kutoa uhai wake uwe fidia ya umati.
Hivyo siku zilizofuata, hasa Ijumaa Kuu, alikabili kwa hiari mateso na kifo kutoka kwa wapinzani wake waliopitia mamlaka ya liwali Ponsio Pilato ili apewe adhabu ya kifo kwa kusulubiwa, na hatimaye akafufuka mtukufu usiku wa kuamkia Jumapili.
Kabla ya hapo Yesu alijumlisha hayo matukio yajayo katika karamu ya mwisho aliyokula pamoja na mitume wake 12, akiwaachia agizo la kufanya daima karamu ya namna hiyo kama ukumbusho wake.
Basi, kuanzia Alhamisi kuu jioni hadi Jumapili ya Pasaka jioni Wakristo[1] wanaadhimisha siku tatu kuu za Pasaka, zinazofanya ukumbusho wa Yesu mteswa, mzikwa na mfufuka[2][3] kama ifuatavyo:
- Alhamisi kuu jioni hadi Ijumaa kuu jioni: siku ya Kristo mteswa
- Ijumaa kuu jioni hadi Jumamosi kuu jioni: siku ya Kristo mzikwa
- Jumamosi kuu jioni hadi Jumapili ya Pasaka jioni: siku ya Kristo mfufuka.
Kuhusiana na Pasaka ya Kiyahudi, ni lazima Juma kuu litokee mwishoni mwa Machi au kabla ya wiki ya mwisho ya Aprili.
Ushahidi wa kwanza kuhusu ibada za pekee za Wakristo wakati huo unapatikana katika "Katiba za Mitume" (kwa Kiingereza: "Apostolical Constitutions", 18, 19), zilizoandikwa katika nusu ya pili ya karne ya 3 hadi karne ya 4. Humo ulaji wa nyama unakatazwa wiki nzima, na mfungo kamili unaagizwa kwa siku za Ijumaa na Jumamosi Kuu.
Barua ya Denis wa Aleksandria (260 BK) inaonyesha taratibu hizo zimeshakuwa desturi.[4]