Ukomeshaji wa Biashara ya Watumwa
From Wikipedia, the free encyclopedia
Ukomeshaji wa biashara ya watumwa ni mchakato au mlolongo wa matukio yaliyopelekea ufutaji au usitishaji wa biashara ya watumwa katika karne ya 19.
Biashara ya watumwa ilikuwa biashara iliyodhalilisha utu wa binadamu, hasa Waafrika ambao ndio waliotumika kwa kiasi kikubwa katika biashara hiyo. Basi, baadhi ya watu Ulaya waliweza kuona madhara mbalimbali yaliyotokana na biashara hiyo hatarishi, na kuamua kuanzisha tapo la kuikomesha. Wengi wao walikuwa watu wa dini waliosukumwa na sababu za ubinadamu.
Baadaye mataifa kama Uingereza yaliongeza bidii katika ukomeshaji wa biashara ya utumwa. Kwa kiasi fulani ukomeshaji wa biashara ya utumwa ulikuwa una manufaa ya kiuchumi kwao, hasa kufuatia matokeo ya mapinduzi ya viwanda yaliyotokea nchini mwao.
Uingereza ukiwa taifa kiongozi katika biashara hiyo, halafu katika zoezi hilo la kuikomesha, ulisaidia kwa kiasi kikubwa katika ukomeshaji wa biashara hii iliyopitia katika bahari ya Atlantiki na ile ya bahari ya Hindi. Si mataifa yote yalikubaliana na matakwa ya Uingereza ya kukomesha biashara ya utumwa, hivyo Uingereza ilipata upinzani kutoka kwa mataifa mengine yaliyokuwa bado yananufaika na biashara hii kama Ufaransa na Ureno.